MICHAEL MTANZANIA

ONESTEPMEDIATZ

Paul Makonda Anafurahia Tuhuma za Cheti Dhidi Yake..!!!



Inabidi wafuatiliaji wa tuhuma hizi tufikie hitimisho hilo. Kuanzia kwenye mitandao,kanisani,runingani,magazetini,redioni hadi mitaani,mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam,Paul Makonda anasemwa kuwa anatumia cheti cha mtu mwingine.

Cheti kinachosemwa ni cheti cha kidato cha nne. Inasemwa kuwa Paul Makonda haitwi hivyo. Jina lake halisi linatajwa kama ni Daudi Albert Bashite. Daudi anasemwa kuwa alifeli kidato cha nne kwa kupata sifuri na hivyo hana cheti

Inasemwa kuwa Daudi akatumia cheti cha kidato cha nne cha Paul Christian kuendelea na masomo na kufika alipofika akijulikana kama Paul Makonda. Kimsingi,kulingana na cheo na hadhi ya Makonda,tuhuma hizi dhidi yake ni nzito sana. 

Uzito wa tuhuma hizo ni mambo ya kijinai yaliyopo na hata masuala ya kimaadili. Tuhuma hizi zinawagusa hata wazazi wake ambao wanamtambua Paul Makonda hivyo badala ya Daudi Albert Bashite anavyopaswa kutambulika kulingana na tuhuma

Paul Makonda hapaswi kuwa kimya. Anapaswa kusema au kutenda jambo kuhusu tuhuma hizi nzito za kijinai za kutumia cheti cha mtu mwingine. Kama tuhuma ni za kweli,Makonda aachie ngazi mara moja na sheria ichukue mkondo wake. Kama tuhuma si za kweli,Makonda awaburuze mahakamani wote wanaozisema tuhuma hizo akiwemo Mch. Gwajima.

Lakini,suluhisho kubwa zaidi ni kuonyesha cheti cha kidato cha nne hadharani kama ilivyofanyika kwa DAS mmoja pale Ikulu ambaye naye alituhumiwa kuhusu elimu yake. Kukaa kimya ni kufurahia. Umaarufu wa kuchafuliwa haufai,Makonda afanye jambo. Tuhuma hizi hazipuuziki kirahisi.

Post a Comment

0 Comments